Tanzania emblem
The United Republic of Tanzania

Prime Minister's Office

Labour, Youth, Employment and Persons with Disability

News

MHAGAMA APONGEZA MAFANIKIO YALIYOFIKIWA KATIKA UJENZI KIWANDA CHA BIDHAA ZA NGOZI CHA KARANGA


Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu anayeshughulikia Sera, Bunge, Kazi, Vijana, Ajira na Wenye Ulemavu Mhe. Jenista Mhagama ametoa pongenzi kwa Jeshi la Magereza na Mfuko wa Hifadhi ya Jamii kwa Watumishi wa Umma (PSSSF) kwa hatua waliyofika katika ujenzi wa kiwanda cha bidhaa za Ngozi cha Karanga.

Akizungumza mara baada ya kukagua maendeleo ya mradi huo wa ujenzi wa kiwanda hicho uliopo Moshi, Mkoani Kilimanjaro ambapo hatua za ujenzi umefikia asilimia 97 Waziri Mhagama alieleza kuwa mikakati ya Serikali ya Awamu ya Tano inayoongozwa Dkt. John Pombe Magufuli, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ni kuendeleza uchumi wa Taifa kupitia Viwanda.


“Mradi huu wa ujenzi wa Kiwanda cha kuzalisha bidhaa za Ngozi hapa Karanga ni mmoja ya utekelezaji wa miradi ya kimkakati ambayo inatekelezwa na Serikali ya Awamu ya Tano na utakuwa mfano wa kuigwa na mataifa mengine utakapoanza uzalishaji wa bidhaa za Ngozi ambazo zitakuwa zinazalishwa hapa nchini,” alieleza Mhagama.

“Nimeridhika na kasi ya ujenzi wa mradi huu, na nitoe pongezi zangu kwa Jeshi la Magereza linalosimamia ujenzi wa mradi huu kwa kushirikiana na Mfuko wa Hifadhi ya Jamii (PSSSF) hatua mliyofikia kwa kweli ni nzuri,”


Alisema Mhagama Alifafanua kuwa, Kiwanda hicho kitakavyo kamilika mapema kitakuwa na manufaa makubwa kwa taifa ikiwemo kutoa fursa za ajira kwa Watanzania pamoja na kuongeza mapato ya Serikali kupitia bidhaa zitakazokuwa zinazalishwa na kiwanda hicho kuuzwa ndani na nje ya nchi.


Aliongeza kuwa kukamilika kwa majengo manne ya msingi katika kiwanda hicho ina ashiria kuwa hatua iliyobaki sasa ni kusimikwa mitambo ya uchakataji wa ngozi ili kiwanda hicho kiweze kuanza kazi ya uzalishaji haraka.

Aidha, Waziri Mhagama ametoa maagizo kwa Mkurugenzi wa Mfuko wa Hifadhi ya Jamii kwa Watumishi wa Umma kuhakikisha anasimamia kwa karibu matumizi ya fedha ya mradi huo.


“Ujenzi wa mradi huu umefikia asilimia 97 na matumizi ya fedha yanaridhisha ikionesha kwenye kumbukumbu zenu kuwa kuwa hadi sasa asilimia 63 ya malipo yamekishafanyika, hivyo suala la ‘Value for Money’ limeweza kutekelezwa katika mradi huu,” alisema Mhagama.

Pia Mheshimiwa Mhagama alielezea namna alivyofurahishwa na utekelezaji wa mafunzo ya vitendo sehemu za kazi ambayo yamekuwa ni chachu ya kuwawezesha vijana kukuza ujuzi walionao.

“Katika mradi wa ujenzi wa kiwanda hiki nimefurahi kuona vijana ambao wanataaluma ya uhandisi wameweza kushiriki na kutoa mchango wao katika mradi huu wa muhimu kwa taifa ambao umewawezesha kupata ujuzi na wameonyesha namna walivyojitoa katika kujenga nchi yao,” alisema Mhagama.


Kwa Upande wake Mkuu wa Magereza Mkoa wa Kilimanjaro, RPO Dkt. Miraji Katumbily alieleza kuwa ujenzi wa mradi huo umefikia asilimia 97 na hatua iliyobaki sasa ni pamoja na kusimikwa kwa mashine ya uchakataji, kuweka miundombinu ya umeme, vifaa vya TEHAMA na kukamilisha ofisi ili uzalishaji katika kiwanda hicho uanze rasmi.

Naye Mkurugenzi wa Mfuko wa Hifadhi ya Jamii kwa Watumishi wa Umma (PSSSF) Bw. Hosea Kashimba alimuhakikishia Waziri huyo kuwa Ofisi yake kwa kushirikiana na Jeshi la Magereza nchini kuwa watatekeleza maagizo yote yaliyotolewa ili kuhakikisha mradi huo unakamilika bila kuwa na kasoro zozote.


Wakati huo huo, Kijana mmoja wapo anayejitolea kwa mafunzo ya vitendo katika mradi huo Mhandisi Edward Chalamila alimshukuru Waziri kwa Ofisi yake kuweza kutambua umuhimu wa Programu hiyo ambayo imekuwa na manufaa kwa vijana katika kukuza ujuzi wa fani walizozisomea.