Tanzania emblem
The United Republic of Tanzania

Prime Minister's Office

Labour, Youth, Employment and Persons with Disability

News

WAZIRI MHAGAMA ATAKA MAAFISA KAZI NCHINI KUTATUA MIGOGORO KWENYE MAENEO YA KAZI


Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu Sera, Bunge, Kazi, Vijana, Ajira na Watu Wenye Ulemavu Mhe. Jenista Mhagama amewataka maafisa kazi nchini kutatua migogoro inayojitokeza katika maeneo ya kazi huku akieleza kuwa Serikali haitasita kuchukua hatua za kisheria kwa maafisa kazi watakaoshindwa kutekeleza wajibu wao.

Waziri Mhagama, aliyasema hayo hii leo Februari 15, 2021 wakati akifungua mafunzo kazi ya Mpango Mkakati wa Usimamizi wa Sheria za Kazi ambayo yamelenga kuwajengea uwezo maafisa kazi 40 kutoka kwenye mikoa mbalimbali nchini yaliyoandaliwa na Ofisi ya Waziri Mkuu – Kazi, Vijana, Ajira na Wenye Ulemavu kupitia (Idara ya Kazi) kwa kushirikiana na Shirika la Kazi Duniani (ILO).


Alieleza kuwa ili kufikia azima ya serikali ya Tanzania ya viwanda ni lazima ufumbuzi wa changamoto katika maeneo ya kazi upatikane na ili wananchi wafanye kazi katika mazingira salama na kupatiwa haki zao za msingi ni lazima sheria za kazi zisimamiwe na kutekelezwa ipasavyo.

“Mnatambua kwamba Taifa letu linapita katika mageuzi makubwa ya kiuchumi na dhamira yetu ni kukuza viwanda nchini, hivyo kama sisi atujajipanga vizuri kwenye sekta ya kazi migogoro itakuwa mingi na hatutakuwa na tija ya kujenga uchumi wa viwanda. Sheria, Sera na Miongozo inatuelekeza mahali popote palipokuwa na migogoro hakuna tija na tija itapatikana kama tutatekeleza wajibu wetu sawa sawa,” alieleza Waziri Mhagama

“Niwasihi mtumie mafunzo haya kama fursa ya kuleta mabadiliko acheni kufanya kazi kwa mazoea kuna migogoro mingi huko nje nisingependa msubiri yafike kwetu viongozi wakati nyinyi mpo ni wajibu wenu kutatua kero,”alisema Mhagama.

Aliongeza kuwa, sekta ya viwanda inakuwa nchini kwa kasi sana na miradi ya kimkakati inaongezeka katika taifa hili na kila eneo la mradi jipya iwe ni uwekezaji au mradi wa mkakati hilo tayari ni eneo la ajira hivyo kama afisa kazi ni wajibu wako wa moja kwa moja wa kusimamia maeneo hayo.

Katika hatua nyingine Waziri Mhagama aliagiza kutolewa kwa taarifa ya kila robo mwaka kwa kila afisa kazi mkoa kuhusiana na utendaji wake hasa katika utatuzi wa migogoro maeneo ya kazi huku akipongeza mikoa iliyofanya vizuri katika kuchukua hatua za kutafuta suluhu ya migogoro ya masuala ya wafanyakazi.

“Kuna mikoa imefanya vizuri katika kushughulikia matatizo ya wafanyakazi kama vile Geita, Tanga, Iringa, Rukwa, Mtwara na Kilimanjaro niwaombe muongeze nguvu kwa Mbeya, Njombe, Dar es Salaam (Wilaya ya Temeke), Morogoro hamfanyi vizuri sana taarifa zote ninazo sasa kupitia taarifa ya robo ya mwaka kwa mkoa utakojirudia kufanya uzembe tutachukua hatua,” alieleza Waziri Mhagama

“Inasikitisha Viongozi wanatembelea maeneo yenu wanafika mahali wawekezaji, wafanyakazi wanalalamika kwao wakati nyie maafisa kazi mpo, simamieni wajibu wenu kwa kutatua kero mara kwa mara na mkifanya hivyo mtakuwa mmeisaidia ofisi yetu kutimiza wajibu kwenye sekta hii ya kazi na ajira,” alieleza

Aidha Waziri Mhagama alitumia fursa hiyo kuelezea kuwa Ofisi hiyo inatengeneza mfumo wa kielektroniki wa kutoa vibali vya Kazi na Ukaazi kwa wageni, mfumo huu utarahisisha utendaji kazi kwa maafisa kazi kwa kutoa vibali (Online) na mfumo huu utaondoa rushwa na vishoka, tutaweza kutambua ujuzi wa wageni waliopo nchini na pia tutaweza kutambua ujuzi ambao ni haba hapa nchini.

Sambamba na hayo alishukuru Shirika la Kazi Duniani (ILO) kwa namna ambavyo wamekuwa wakishirikiana karibu na Ofisi ya Waziri Mkuu katika kushughulikia masuala mbalimbali kwenye sekta ya kazi na ajira nchini.

Kwa upande wake Mwakilishi kutoka Shirika la Kazi Duniani (ILO), Maridadi Fanuel alisema kuwa mafunzo hayo yamelenga katika maeneo mbalimbali ikiwemo ukuzaji wa ajira zenye staha, masuala ya hifadhi ya jamii, majadiliano ya utatu kukuza uhusiano wa karibu kati ya serikali, vyama vya wafanyakazi na vyama vya waajiri na eneo la mwishi ni haki katika sehemu za kazi.

“Katika kutekeleza suala la usimamizi wa sheria za kazi shirika la Kazi Duniani (ILO), ilipitisha mkataba wa Ukaguzi Na. 81 amabo uliridhiwa na Tanganyika, Mkataba huo ndio ambao umechangia mafuzno hayo kuandaliwa kwa maafisa kazi ili kuwawezesha maafisa kazi na maafisa ukaguzi wanajengewa uwezo katika kutekeleza amjukumu yao kwa mujibu wa sheria,” alifafanua Mwakilishi huyo.

Kwa Upande wake, Naibu Waziri anayeshughulikia masuala ya Kazi, Vijana na Ajira Mhe. Patrobas Katambi alieleza kuwa mpango huu wa mafunzo ni mzuri na utawajengea uzoefu maafisa kazi ambapo wataweza kujiwekea utaratibu mzuri wa utendaji wa kazi zao.

Naye, Naibu Waziri Naibu Waziri, Ofisi ya Waziri Mkuu anayeshughulikia Watu wenye Ulemavu Mhe. Ummy Nderiananga alihimiza suala la ushirikishwaji wa watu wenye ulemavu ili kusaidia kundi hilo kupata ajira na kuifanya jamii kutambua umuhimu wa kuwaajiri hususan kwenye sekta binafsi.

“Kwa upande wa kundi la watu wenye ulamevu bado kuna shida katika suala la ajira sasa ikiwa tunataka kufikia katia malengo ya maendeleo endelevu ifikapo 2025 ni lazima tusimamie kundi hili kwa kuhakikisha wanapata kazi zenye staha na wasibaguliwe kutokana na ulemavu wao wapewe fursa kama wengine ,”alieleza Waziri Ummy.

Kwa Upande wake, Kamishna wa Kazi Brig. Gen. Francis Mbindi alieleza kuwa mafunzo hayo yameshirikisha maafisa kazi wasimamizi wa sheria za kazi pamoja na maafisa kazi waendeshaji wa mashtaka hivyo mafunzo hayo yataimarisha utendaji kazi katika Idara ya Kazi na hatimaye kupunguza malalamiko.