Tanzania emblem
The United Republic of Tanzania

Prime Minister's Office

Labour, Youth, Employment and Persons with Disability

News

Prof. Ndalichako: Rais Samia ameendelea kushusha fursa kwa Watu wenye Ulemavu


Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu, Kazi, Vijana, Ajira na Wenye Ulemavu, Mhe. Prof. Joyce Ndalichako, amesema Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan ameendelea kutoa fursa kwa watu wenye ulemavu ikiwamo kwa kuwajengea vyuo vya ufundi ili kupata ujuzi.

Mhe. Ndalichako ameyasema jijini Dodoma Juni 28, 2023 kwenye hafla ya chakula cha mchana na viongozi wa watu wenye ulemavu aliyoandaliwa na Mbunge wa Viti maalum(CCM) Mhe. Khadija Taya kwa ajili mwamko wa kuchangamkia fursa zilizopo kwenye maeneo yao.

Amesema Rais Samia ametoa zaidi ya Sh.Bilioni tatu kwa ajili ya kufanya ukarabati vyuo vya watu wenye ulemavu vitano ili kupata ujuzi.

“Huu ujuzi wanaopata moja kwa moja unawasaidia kujikwamua kiuchumi kutokana na ufanisi uliopo kwenye vyuo hivi, Mhe. Rais ametoa Sh.Bilioni tatu katika mwaka wa fedha 2022/23 ili kujenga vyuo vitatu katika Mkoa wa Ruvuma, Songwe na Kigoma na katika bajeti ya 2023/24 zimetengwa Sh.Bilioni tatu ili kuendeleza ujenzi,”amesema.

Kuhusu mikopo, amesema watu wenye ulemavu wamekuwa wakipata mikopo kupitia asilimia mbili ya mapato ya ndani ya Halmashauri na kutoa wito kuchangamkia fursa hiyo kwa kuwa Rais ametengeneza fursa kwa ajili yao.

Kadhalika, Waziri Ndalichako amesema kwa mwaka 2023/24 serikali imetenga Sh.Milioni 62 kwa ajili ya kununua malighafi za kutengenezea mafuta ya watu wenye ualbino ili kuongeza upatikanaji wa mafuta hayo na kwa gharama nafuu.

Naye, Mhe. Mbunge Taya amesema zipo fursa nyingi za watu wenye ulemavu za kujikwamua kiuchumi wanazopaswa kuzichangamkia ikiwamo zilizopo kwenye sheria ya ununuzi wa umma inayowapa fursa ya asilimia 30 ya zabuni kwa makundi maalum ya wanawake, vijana na wenye ulemavu.