Tanzania emblem
The United Republic of Tanzania

Prime Minister's Office

Labour, Youth, Employment and Persons with Disability

News

Kamati ya Bunge yashauri Tume ya Usuluhishi na Uamuzi Kuongezewa Bajeti


Mwenyekiti wa Kamati ya Kudumu ya Bunge na Ustawi na Maendeleo ya Jamii Mhe. Fatuma Toufiq ameishauri serikali kuiongezea bajeti Tume ya Usuluhishi na Uamuzi(CMA) ambayo ipo chini ya Ofisi ya Waziri Mkuu Kazi, Vijana, Ajira na Wenye Ulemavu ili iweze kutekeleza majukumu yake kwa ufanisi na wakati.

Ameyasema hayo Oktoba 18, 2023 Jijini Dodoma wakati wa kikao cha Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Ustawi na Maendeleo ya jamii baada ya kupokea Taarifa ya utekelezaji ya majukumu ya Tume ya Usuluhishi na Uamuzi (CMA).

“ kwa mwaka 2022-2023 tume imesajili kesi zaidi ya 20,156 hivyo inahitajika ipatikane bajeti ya kutosha ili tume hiyo iweze kufanya shughuli zake kwa ufanisi na upana zaidi”

Aidha Mhe. Taufiq ameisistiza Tume kujitangaza na kutoa elimu kupitia vyombo vya Habari ili jamii waweze kutambua shughuli zinazofanywa na taasisi hiyo vilevile ameshauri tume ijifunze kutoka kwenye Nchi zilizoendelea ilikupata uelewa na kujua njia rahisi wanazotumia katika utatuzi wa migogoro ya kikazi.

Kwa upande wa Naibu Waziri Ofisi ya Waziri Mkuu, Kazi, Vijana, Ajira na Wenye Ulemavu Mhe. Patrobas Katambi amesema kuna umuhimu wa kuwa na ofisi nchi nzima zitakazoweza kurahisisha upatikanaji wa huduma za tume kwa haraka na urahisi kwa kuwafikia wafanyakazi nchi nzima kwenye utatuzi wa migogoro ya kikazi.

Naye Katibu Mkuuwa Ofisi hiyo Mhandisi Cyprian Luhemeja ameiahidi kamati kuwa Ofisi hiyo itaendelea kuisimamia Tume ya Usuluhishi na Uamuzi kuzingatia ushauri na maoni ya kamati hiyo.

Awali Mkurugenzi wa Tume ya Usuluhishi na Uamuzi (CMA) Mhe. Usekelege Mpulla amesema Tume imefanikiwa kutatua migogoro ndani ya siku 1 hadi 30 hivyo kwa mwaka 2022-2023 tume imesajili migogoro 20,156 kwa ngazi ya Usuluhishi ni sawa na 58% ya Usuluhishi wake na kwa ngazi ya Uamuzi migogoro 8,397 ilisajiliwa sawa na 65% ya Uamuzi.