Tanzania emblem
The United Republic of Tanzania

Prime Minister's Office

Labour, Youth, Employment and Persons with Disability

News

Luhemeja ataka Mifuko ya Hifadhi ya Jamii kuwekeza kwenye miradi ya uzalishaji


Katibu Mkuu, Ofisi ya Waziri Mkuu, Kazi, Vijana, Ajira na Wenye Ulemavu, Mhandisi Cyprian Luhemeja ameitaka mifuko ya hifadhi ya jamii kuendelea kuwekeza kwenye miradi ya uzalishaji ili kuchochea uchumi na fursa za ajira nchini.

Akizungumza Novemba 2, 2023 alipokagua maendeleo ya ujenzi wa kiwanda cha sukari Mkulazi mkoani Morogoro, Mhandisi Luhemeja amemshukuru Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kutoa kibali na kuridhia ujenzi huo na kwamba uwekezaji wa aina hiyo una faida kubwa kiuchumi na unatarajia kutoa ajira zaidi ya 10,000 kwa watanzania.

“Uwekezaji wa miradi ya uzalishaji kama huu wa kiwanda cha Mkulazi unaongeza ajira na kukuza uchumi, lakini pia kukamilika kwake kutasaidia kupunguza changamoto ya upungufu wa sukari uliopo nchini na kuondoa uagizaji wa sukari kutoka nje ya nchi,”amesema.

Naye, Mwenyekiti wa Bodi ya Kampuni Hodhi ya Mkulazi, Dkt. Hildelitha Msita ameahidi Bodi yake itatekeleza maelekezo aliyotoa Katibu Mkuu Luhemeja ikiwamo mpango wa kuongeza eneo la mashamba kwa ajili ya kilimo cha miwa.

Kadhalika, Mkurugenzi Mkuu wa Mfuko wa Taifa wa Hifadhi ya Jamii (NSSF), Masha Mshomba, amesema NSSF itaendelea kutoa ushirikiano kwa Mkulazi ili kuhakikisha kiwanda hicho kinaanza uzalishaji huku Mwakilishi wa Shirika la Uzalishaji Mali (SHIMA) Muyengi Bulilo, ameahidi kuendelea kuhakikisha ulinzi na usalama kwenye eneo hilo.

Awali, akitoa taarifa kuhusu maendeleo ya mradi huo, Afisa Mtendaji Mkuu wa kampuni Hodhi ya Mkulazi, Selestine Some amesema kiwanda hicho kina uwezo wa kuzalisha tani 75,000 za sukari kwa mwaka na kinatarajia kuanza uzajishaji wa tani 50,000 za sukari.