Tanzania emblem
The United Republic of Tanzania

Prime Minister's Office

Labour, Youth, Employment and Persons with Disability

News

MHE. IKUPA AWATAKA WARATIBU WA MADAWATI YA WATU WENYE ULEMAVU KUTATUA CHANGAMOTO ZA WENYE ULEMAVU NCHINI


MHE. IKUPA AWATAKA WARATIBU WA MADAWATI YA WATU WENYE ULEMAVU KUTATUA CHANGAMOTO ZA WENYE ULEMAVU NCHINI

NA MWANDISHI WETU:

Naibu Waziri Ofisi ya Waziri Mkuu (Watu wenye Ulemavu) Mhe.Stella Ikupa amewataka waratibu wa madawati ya watu wenye ulemavu kuhakikisha wanatatua changamoto zinazo wakabili wenye ulemavu nchini.

Akizungumza wakati wa ufunguzi wa warsha hiyo Waziri Ikupa alieleza kuwa madawati haya ni muhimu sana katika mustakabali mzima wa masuala ya watu wenye ulemavu. Kupitia Sheria imeonekana upo umuhimu wa kuwa na haya madawati kutokana na changamoto zinazowakabili watu wenye ulemavu.

“Kupitia mafunzo haya yataweza kuwajengea uelewa lakini pia kutambua fursa zipi zilizopo katika wizara au taasisi anayotoka na ni jinsi gani zinaweza kuwafikia watu wenye Ulemavu.” Alisema Ikupa

Akitolea mfano Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano kuhusu suala la miundombinu wamekuwa wakifuatilia vipi watu wenye ulemavu katika kutumia usafiri wa anga pasipo kuwa na usumbufu wowote.

Aidha alitoa rai kuwa madawati haya yakazingatie sana mafunzo watakayopata na kuyafanyia kazi ili kuhakikisha changamoto za watu wenye ulemavu zinapungua.

Kwa upande wake Mwenyekiti wa Shirikisho la Vyama vya Watu wenye Ulemavu Tanzania (SHIVYAWATA) Bi. Ummy Nderiananga alifafanua umuhimu wa mafunzo hayo kwa waratibu wa dawati la watu wenye ulemavu kuwa wataweza kubadilishana mawazo mbalimbali na kushauriana nini kifanyike.

“Ninaishukuru Serikali kwa kuendelea kutambua na kuwajali watu wenye ulemavu. Hivyo ni vyema kila mtu sasa aweze kuthamini na kujali kundi hili la watu wenye ulemavu sambamba na kutatua changamoto zao.” alisema Nderiananga.

Naye Kaimu Mkuu wa Kitengo cha Wenye Ulemavu Ofisi ya Waziri Mkuu Bw. Jacob Mwinula alieleza kuwa Watu wenye ulemavu wamekuwa wakikumbana na changamoto mbalimbali ikiwemo masuala ya ajira, elimu, afya, n.k. Hivyo uwepo wa madawati hayakutasaidia kuwa na ushirikiano wa pamoja kwa kuelimishana na kushauriana ili kuhakikisha masuala ya watu wenye ulemavu yanazingatiwa katika jamii.

“Ili kumaliza changamoto za watu wenye ulemavu tunahitajika kuwa na juhudi za pamoja na kupitia madawati haya ambayo yatakuwa yakitujengea uelewa wa kutatua changamoto za watu wenye ulemavu na kuhakikisha zinapungua kwa kiasi kikubwa.” Alisema Mwinula.

Lengo kuu la warsha hiyo ililikuwa ni kuwajengea uwezo Waratibu wa madawati ya Watu wenye Ulemavu kutoka katika Wizara na Taasisi mbalimbali.

MWISHO