Tanzania emblem
The United Republic of Tanzania

Prime Minister's Office

Labour, Youth, Employment and Persons with Disability

News

Mhe. Katambi: Ulinzi bandarini, mipakani na viwanja vya ndege ni salama


Naibu Waziri, Ofisi ya Waziri Mkuu, Kazi, Vijana, Ajira na wenye Ulemavu Mhe. Patrobas Katambi amesema hali ya ulinzi katika maeneo ya bandari, mipaka ya nchi na katika viwanja vya ndege ni salama.

Aidha, amesema katika maeneo hayo ukaguzi unaofanyika ni wa kisasa ambapo vifaa vya Kielektroniki vina uwezo wa kubaini uhalifu unaoweza kujitokeza.

Mhe. Katambi amebainisha hayo Januari 5, 2024 Jijini Dar es salaam alipofanya ziara katika Uwanja wa Ndege wa kimataifa wa Julius Nyerere na maeneo ya bandarini kwa ajili ya kukagua hali ya ulinzi na usalama katika maeneo hayo na kuagalia utoaji huduma katika maeneo hayo.

“Tanzania siyo sehemu salama ya kusafirisha binadamu kwenda kutumikishwa nje ya nchi na wala siyo salama kupita na madawa ya kulevya na mambo mengine ambayo ni kinyume na sheria.” amesema

Vile vile, Mhe. Katambi amekanusha taarifa ambazo hivi karibuni zimekuwa zikisambaa kupitia mitandao ya kijamii zikielezea uwepo wa Watoto na Watu Wenye Ulemavu wanao safirishwa kupitia maeneo hayo kwenda kutumikishwa nje ya Nchi ikiwemo Kenya.

Awali akitoa taarifa kuhusiana na tetesi za watu wenye ulemavu kusafirishwa kwa ajili ya utumikishwaji kupitia uwanja wa ndege, Naibu Kamishina wa Uhamiaji (DCI), Juliette Sagamiko amesema mifumo ya ukaguzi na usimamizi nchini ipo vizuri na hakuna mwenye ulemavu aliyesafirishwa kwenda nchi jirani kwa ajili ya kutumikishwa.

Naye, Katibu Mkuu wa Shirikisho la Vyama vya Watu wenye Ulemavu (SHIVAWATA), Jonas Lubago amempongeza Mhe. Rais, Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kuendelea kuwajali Watu wenye Ulemavu. Pia, ametumia fursa hiyo kukemea watu wenye tabia ya kuwatumikisha wenye Ulemavu kuacha tabia hiyo.

MWISHO