Tanzania emblem
The United Republic of Tanzania

Prime Minister's Office

Labour, Youth, Employment and Persons with Disability

News

MIFUKO YA UWEZESHAJI WANANCHI KIUCHUMI YAPEWA SIKU 45 KUTENGENEZA MPANGO MKAKATI WA PAMOJA


Mifuko na Program za Uwezeshaji Wananchi Kiuchumi imepewa siku 45 kutengeneza mpango mkakati wa pamoja utakaoelekeza vipaumbelele vya kitaifa vya kisekta kutokana na Shughuli zaUchumi zilizopo katika maeneo mbalimbali nchini.

Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera, Bunge, Kazi, Vijana, Ajira na Wenye Ulemavu), Mhe. Jenista Mhagama ameyabainisha hayo leo jijini Dodoma wakati akifungua kikao kazi cha Mifuko na Programu za Uwezeshaji Wananchi Kiuchumi.

Waziri Jenista amesema kuwa dhumuni la Serikali ni kuiweka mifuko hiyo iweze kufanya kazi kwa kushirikiana kwani imebainika kuwa kila mfuko unafanya kazi katika uwanja wake pasipo ushirikiano wa pamoja na Mifuko au Programu zingine hali inayopelekea kutokea kwa changamoto katika kufikia Malengo ya Dira ya Maendeleo ya Taifa ya 2025.

“Ili kuwafikia wananchi wengi ni lazima tufanye maamuzi magumu ya pamoja yatakayotuwezesha tuwe na maamuzi ya pamoja katika kutengeneza nchi kwenda katika lengo la kimkakati wa taifa hivyo natoa siku 45 kwa wahusika kukamilisha mpango kazi wa Taifa wa Uwezeshaji Wananchi Kiuchumi,” alisema Waziri Jenista.

Mpango kazi huo utaiwezesha mifuko hiyo kujiratibu na kutengeneza mfumo ambao utaenda sawa na muelekeo wa serikali pamoja na kuwawezesha wananchi kunufaika na mifuko hiyo sawa sawa na malengo yaliyokusudiwa.

Ameongeza kuwa pamoja na kutengeneza mpango huo, lazima mifuko na Programu hizo ziwekwe kwa makundi yanayofanana ili kurahisisha utendaji kazi wa mifuko hiyo ambayo itawezesha mageuzi makubwa ya kiuchumi.

Aidha, katika kutekeleza masuala hayo kwa ufanisi, Waziri Jenista amependekeza kuundwa kwakikosi kazi kitakachoshirikiana kwa pamoja katika maandalizi ya mpango huo kitakachojumuishawawakilishi kutoka katika Taasisi za Mifuko na Programu za Uwezeshaji ambapo Idara ya Uwezeshaji na Maendeleo ya Sekta Binafsi iliyopo Ofisi ya Waziri Mkuu itawajibika katika Maandalizi ya Hadidu za Rejea pamoja na Muda wa kimkakati katika kila hatua ya maandalizi ya kazi hiyo.

Baraza la Taifa la Uwezeshaji Wananchi Kiuchumi imekuwa ikiratibu Programu na Mifuko 45 ya Uwezeshaji Wananchi Kiuchumi iliyoanzishwa kwa lengo kuu la kupanua wigo wa utoaji huduma za kifedha pamoja na huduma nyingine za uwezeshaji wananchi kiuchumi ili kuwafanya washiriki kikamilifu katika uchumi wa Nchi.

Naibu Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu, Kazi, Vijana na Ajira, Mhe. Anthony Mavunde akizungumza wakati wa kikao kazi baina ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu Sera, Bunge, Kazi, Vijana, Ajira na Wenye Ulemavu, Mhe. Jenista Mhagama (hayupo pichani) na watendaji wa mifuko ya uwezeshaji wananchi kiuchumi leo jijini Dodoma.

Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu Sera, Bunge, Kazi, Vijana, Ajira na Wenye Ulemavu, Mhe. Jenista Mhagama (kushoto) akipongezwa na Katibu Mtendaji wa Baraza la Taifa la Uwezeshaji Wananchi Kiuchumi (NEEC), Beng’i Issa mara baada ya kuwasilisha hotuba ya ufunguzi wa kikao kazi cha watendaji wa Mifuko ya uwezeshaji wananchi kiuchumi Jijini Dodoma.