Tanzania emblem
The United Republic of Tanzania

Prime Minister's Office

Labour, Youth, Employment and Persons with Disability

News

Naibu Waziri Katambi awabana Wawekezaji wanaokiuka Sheria za Kazi


Naibu Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu (Kazi, Vijana, Ajira na Wenye Ulemavu), Patrobas Katambi, amefanya ziara katika viwanda vya Mkoa wa Dar es Salaam ambapo ameeleza kutoridhishwa na hali ya utekelezaji wa Sheria za Kazi, Usalama na afya pamoja na hifadhi kwa jamii katika baadhi ya viwanda.

Akizungumza mara baada ya kufanya ukaguzi wa mifumo ya usalama na afya na uzingatiaji wa sheria za kazi katika kiwanda cha Colourful Industry Limited kilichopo Buza-Temeke jijini Dar es Salaam kinachozalisha bidhaa za plastiki ikiwemo mifagio na vifungashio, Naibu Waziri Katambi, ameutaka uongozi wa kiwanda hicho kuboresha mazingira ya kazi pamoja na kushughulikia changamoto mbali mbali za wafanyakazi ndani ya siku 14.

“Nimetembelea sehemu mbali mbali za uzalishaji katika kiwanda hiki na kubaini ukiukwaji mkubwa wa taratibu za usalama na afya mahali pa ikiwemo wafanyakazi kutopatiwa vifaa vya kujikinga na vihatarishi vya magonjwa na ajali. Hali ya mazingira ya kazi sio nzuri kuna mzunguko finyu wa hewa na hata mwanga hautoshelezi,” amesema Katambi na kuongeza:

“Ukiukwaji wa haki nyingine za wafanyakazi ikiwemo ujira mdogo, wafanyakazi kulazimishwa kufanya kazi kwa zaidi ya masaa yanayoruhusiwa kisheria bila kupatiwa malipo ya ziada pamoja na kutowasilisha michango ya wafanyakazi katika mifuko ya hifadhi kwa jamii.”

Aidha, Katambi alitembelea kiwanda cha Steel Masters Limited kilichopo Chang’ombe jijini Dar es Salaam kinachozalishaji bidhaa za chuma na kufanya ukaguzi wa maeneo ya uzalishaji pamoja na masuala mengine yanayohusu utekelezaji wa sheria za kazi, usalama na afya na hifadhi kwa jamii.

Akiwa katika kiwanda hicho halikadhalika alibaini mapungufu katika utekelezaji wa sheria tajwa ikiwemo wafanyakazi kutokingwa na kilele zinazalishwa na mitambo pamoja na taarifa zisizojitosheleza kuhusiana na uwasilishwaji wa michango katika mifuko ya hifadhi kwa jamii.

Naibu Waziri huyo mwenye Dhamana ya Masuala ya Kazi aliwaagiza maafisa kutoka Taasisi chini ya Ofisi ya Waziri Mkuu kurudi tena katika kiwanda hicho kwa ukaguzi zaidi na kushauri namna bora zaidi itakayowezesha kiwanda hicho kutekeleza sheria za kazi, usalama na afya pamoja na hifadhi kwa jamii.

Kwa upande wake mwakilishi wa Kampuni ya Steel Masters Limited, Gajendra Narendra, amemshukuru Naibu Waziri kwa kufanya ziara katika kiwanda chao na kutoa ushauri na maelekezo mbali mbali.

“Tupo tayari kuyafanyia kazi maelekezo yaliyotolewa na Mheshimiwa Naibu Waziri, tunamuahidi kwamba tutayafanyia kazi kwa mwongozo wa wataalam wake na tupo tayari kumwalika tena baada ya kukamilisha maboresho hayo,” ameeleza Bw. Narendra.

Taasisi zilizoambatana na Naibu Waziri Katambi katika ziara hiyo ni pamoja na Wakala wa Usalama na Afya Mahali pa Kazi (OSHA), NSSF, WCF pamoja na Idara ya Kazi.