Tanzania emblem
The United Republic of Tanzania

Prime Minister's Office

Labour, Youth, Employment and Persons with Disability

News

Prof. Ndalichako azindua Mradi wa Kukuza Kazi za Staha katika zao la Pamba


Waziri wa Nchi - Ofisi ya Waziri Mkuu, Kazi, Vijana, Ajira na Wenye Ulemavu Mhe. Prof. Joyce Ndalichako amezindua mradi wa kukuza kazi zenye staha katika zao la pamba unaolenga kuongeza thamani ya uzalishaji wa zao hilo na kulinda haki za Watoto.

Prof. Ndalichako amezindua Mradi huo Oktoba 21, 2023 Jijini Dar es salaam kwenye kongamano la mwaka la Maafisa kazi na uzinduzi wa mradi wa kazi zenye tija katika sekta ya pamba nchini Tanzania.

Amesema mazingira ya uzalishaji wa zao hilo kwa kiasi kikubwa yanasababisha uwepo wa vitendo vya ukiukaji wa haki za watoto ikiwemo utumikishwaji.

“Mhe. Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan anapenda kuona Watanzania wanakuwa na Ustawi ikiwa ni pamoja na kuongezeka kwa thamani ya Pamba inayozalishwa kwa kuzingatia ulinzi wa haki za Watoto” amesema

Amesema kuupitia Mradi huo Serikali inategemea kuongezeka kwa ufanisi wa utekelezaji wa Sera na Sheria kwa kuboresha ulinzi wa Watoto, kuongezeka kwa wigo wa Kinga ya Jamii, kusaidia uanzishwaji wa Mpango Kazi wa Taifa dhidi ya Utumikishwaji wa Mtoto na Uimarishaji wa uzalishaji wa pamba bora na yenye thamani katika soko la Dunia

Aidha, amewaasa wasimamizi na wahusika watakaotekeleza Mradi huo kuzingatia weledi na maadili ya kazi katika kutekeleza Mpango wa Utekelezaji ulioandaliwa ili rasilimali zilizotolewa ziweze kutumika kama ilivyokusudiwa.

Kwa upande wake Katibu Mkuu Ofisi hiyo Mhandisi Cyprian Luhemeja amesema taarifa ya hali ya uchumi kwa mwaka 2021/2022 imebainisha Utumikishwaji wa Mtoto nchini umefikia Asilimia 24.9 na sekta ya kilimo inaongoza katika maeneo ya vijijini ambapo wakulima hutumia watoto wao kama nguvukazi ili kuondoa gharama za uendeshaji.

Mradi huo unafadhiliwa na Serikali ya Brazilin na Shiriki la Kazi Duniani (ILO) utakao gharimu Dola za Kimarekani 558,170 na utatekelezwa kwa miaka miwili katika Wilaya ya Meatu Mkoani Simiyu.