Tanzania emblem
The United Republic of Tanzania

Prime Minister's Office

Labour, Youth, Employment and Persons with Disability

News

Serikali itaendelea kulinda maslahi ya Vijana - Mhe. Katambi


Naibu Waziri, Ofisi ya Waziri Mkuu - Kazi, Vijana, Ajira na Wenye Ulemavu, Mhe. Patrobas Katambi amesema Serikali ya Awamu ya Sita inayoongozwa na Mhe. Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan inawajali vijana na itaendelea kulinda maslahi yao wakati wote.

Pia, Mheshimiwa Katambi ametoa wito kwa vijana nchini kuchangamkia fursa zinazotolewa na serikali kupitia programu za kuwawezesha na miradi mikubwa ya kimkakati ili waweze kujikwamua kiuchumi na kutatua changamoto ya ajira miongoni mwa vijana.

Mhe. Katambi ameyasema hayo leo Julai 8, 2023 wakati akifungua bonanza la michezo la vijana wa mradi wa USAID KIJANA NAHODHA unaotekelezwa na Shirika la T-MARC Tanzania, ambalo limefanyika katika uwanja wa Jamhuri Mkoani Morogoro.

Amesema kuwa, Serikali imedhamiria kuwajengea vijana uwezo wa masuala ya kiuchumi, kijamii, kisiasa, utamaduni na kiafya ili kuwa na nguvukazi imara.

“Michezo ni afya na michezo ni maisha, hivyo niwahamasishe vijana kuchangamkia fursa hii ili kuimarisha afya zenu kimwili na kiakili kwa kujenga taifa lenye nguvu kazi ya vijana walio imara na pia kutumia michezo hii kama chanzo cha ajira,” amesema

Vile vile, Naibu Waziri Katambi amesema Mradi huo wa USAID Kijana Nahodha ni miongoni mwa jitihada zinazochukuliwa na serikali kwa kushirikiana na mataifa na wadau wa maendeleo nchini katika kuimarisha ustawi na maendeleo ya vijana kiuchumi na kijamii.

Akizungumza awali, Mkurugenzi wa mradi huo, Dkt. Tuhuma Tulli, amesema mradi huo unafadhiliwa na USAID na unalenga kusaidia vijana wenye umri wa miaka 15 hadi 25 hususan walio nje ya mfumo rasmi wa elimu kwa kuwapatia mafunzo ya ufundi stadi, ujuzi, ujasiriamali, kilimo, masuala ya afya, uraia na uongozi.

“Bonanza hili ni sehemu ya kuhamasisha vijana wetu kuchangamkia fursa mbalimbali zitakazo wainua kiuchumi na kuwafanya kuwa raia bora wa taifa lao na viongozi bora baadae,” amesema