Tanzania emblem
The United Republic of Tanzania

Prime Minister's Office

Labour, Youth, Employment and Persons with Disability

News

UJENZI KIWANDA KIPYA CHA BIDHAA ZA NGOZI CHA KARANGA WAPAMBA MOTO


Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu anayeshughulikia Sera, Bunge, Kazi, Vijana, Ajira na Wenye Ulemavu Mhe. Jenista Mhagama amepongeza kasi ya ujenzi wa Kiwanda kipya cha Bidhaa za Ngozi cha Karanga kinachojegwa kwa Ubia baina ya Mfuko wa Hifadhi ya Jamii kwa Watumishi wa Umma (PSSSF) na Jeshi la Magereza.

Waziri Mhagama ameyasema hayo Februari 8, 2020 wakati wa ziara ya kukagua maendeleo ya Ujenzi wa Kiwanda kipya cha Bidhaa za Ngozi cha Karanga kilichopo Moshi, Mkoani Kilimanjaro ambapo asilimia 60 ya ujenzi wa kiwanda hicho imekamilika.

Akiwa katika ziara hiyo amethibitisha kuridhika kwa hatua za awali zilizofikiwa na kueleza azma ya Serikali katika kuhakikisha kiwanda hicho kinakamilika kwa wakati kwani kina manufaa makubwa kwa taifa ikiwemo kutoa fursa za ajira na kuchangia katika ukuaji wa pato la taifa.

“Nimeridhishwa na kasi ya ujenzi wa mradi huu, na niwaombe mwendelee kutekeleza majukumu yenu usiku na mchana na mjipange kukamilisha kwa wakati, ninaamini kama mgekuwa mmejipanga mapema mradi huu ungekuwa umekamilika hivyo mjipange vizuri kwa kuwa uwezo mnao,” alisema Mhagama

Alifafanua kuwa kiwanda hicho kikikamilika maapema kitaiwezesha Tanzania kuufikia azma inayoitaka ya uchumi wa viwanda kwa kuwa bidhaa bora na zitakazozalishwa katika kiwanda hicho.

“Tunataka Kiwanda hiki kiwe ni mfano wa kuigwa katika Afrika Mashariki kwa kuwa kitazalisha bidhaa zitakazo uzika ndani na nje ya nchi, hivyo mapato yatakayopatikana yataleta faida kubwa kwenye ukuaji wa uchumi wa nchi,” alisema Mhagama.

Aidha Waziri Mhagama alitoa maagizo kwa wasimamizi na Mkandarasi wa mradi huo na kuwataka kuandaa mpango kazi utakawawezesha kufuatilia kila hatua inayoendelea kwenye ujenzi wa kiwanda hicho, pia kuandaa mapema mpango mkakati wa biashara na masoko utakao wezesha bidhaa zitakazozalishwa zinapata soko la uhakika.

Sambamba na hayo Mhe. Mhagama amemwagiza Katibu Mkuu, Ofisi ya Waziri Mkuu – Kazi, Vijana, Ajira na Wenye Ulemavu kukutana na Wizara ya Viwanda na Biashara pamoja na Makampuni na Wadau wa sekta ya ngozi ili kuangalia upatikanaji wa ngozi bora kwa ajili ya matumizi ya kiwanda hicho ili kitakapokamilika kianze uzalishaji haraka.

Kwa Upande wake Katibu Mkuu, Ofisi ya Waziri Mkuu, Kazi, Vijana, Ajira na Wenye Ulemavu Bw. Andrew Massawe amesema kuwa maagizo yaliyotolewa na Waziri alipofanya ziara Januari 15 mwaka huu ataendelea kuyasimamia ili kasi ya ujenzi wa kiwanda hicho kiweze kukamilika kama ilivyokusudiwa.

Wakati huo huo Mhandisi wa mradi huo, SP. Julius Sukambi akitoa taarifa ya utekelezaji wa mradi alieleza kuwa hatua iliyofikiwa sasa ni kutokana na utekelezaji wa maagizo yaliyotolewa na Waziri ikiwemo suala la kuongeza nguvu kazi.

“Hivi sasa ujenzi unafanyika masaa 24 yani Usiku na Mchana kwa kutumia wataalam wa Jeshi la Magereza, Mafundi wabobezi na wafungwa ili kukamilisha ujenzi kwa wakati uliokusudiwa,” alisema Sukambi

Naye Mkurugenzi Mkuu wa Mfuko wa Hifadhi ya Jamii kwa Watumishi wa Umma, Ndg. Hosea Kashimba alisema kuwa tayari Ofisi yake imeshafika hatua za mwisho kwa ajili ya kupokea Mashine za kutengeneza viatu vitakavyo kuwa vikizalishwa kwenye kiwanda hicho kilichopo Moshi, Mkoani Kilimanjaro.