Tanzania emblem
The United Republic of Tanzania

Prime Minister's Office

Labour, Youth, Employment and Persons with Disability

News

Vyuo 28 kutoa Mafunzo ya Uanagenzi kwa Vijana 3,765


Ofisi ya Waziri Mkuu, Kazi, Vijana, Ajira na Wenye Ulemavu imesaini makubaliano na vyuo vya ufundi 28 vitakavyotoa mafunzo ya uanagenzi awamu ya pili kwa vijana 3,765 wakiwamo na wenye ulemavu.

Mkurugenzi wa Idara ya Ajira na Ukuzaji Ujuzi wa Ofisi hiyo, Ally Msaki ameyasema hayo kwenye kikao cha kusaini makubaliano ya kutoa mafunzo hayo yaliyofanyika Mei 12, 2023 jijini Dodoma.

Msaki amesema mafunzo hayo yataanza kutolewa hivi karibuni na kuwataka wawakilishi wa vyuo hivyo kuhakikisha wanasimamia utoaji wa mafunzo hayo kwa ufasaha kulingana na elimu ya usimamizi waliyopata kutoka Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) na Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (TAKUKURU).

“Haya mafunzo ni ya awamu ya pili katika mwaka wa fedha 2022/23 ambao tulipanga kuwawezesha vijana 11,525 na kwenye awamu ya kwanza tayari vijana 7,760 wamenufaika, ”amesema.

Amefafanua kuwa mafunzo hayo ni ya miezi sita na fani zinazotolewa ni ufundi umeme wa majumbani na viwandani, umeme wa jua, useremala, ufundi magari, umeme wa magari, uchomeleaji na uungaji vyuma, utengenezaji wa vifaa vya aluminium, upishi, uhudumu wa hoteli na vinywaji, ushonaji, uchenjuaji wa madini, ufundi bomba, ufundi uashi, uwekaji wa terazo na marumaru, ufundi viyoyozi na majokofu.