Tanzania emblem
The United Republic of Tanzania

Prime Minister's Office

Labour, Youth, Employment and Persons with Disability

News

Waziri Ndalichako awataka wadau wa sekta ya Umma kushirikiana kuimarisha Usalama na Afya Mahali pa Kazi


Wito umetolewa kwa wadau wa sekta ya umma kushirikiana kikamilifu na Wakala wa Usalama na Afya Mahali pa Kazi (OSHA) kuimarisha mifumo ya usalama na afya mahali pa kazi katika maofisi na miradi ya Serikali.

Wito huo umetolewa na Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu -Kazi, Vijana, Ajira na Wenye Ulemavu, Mhe. Prof. Joyce Ndalichako alipokuwa akifungua mafunzo maalum ya usalama na afya yaliyoandaliwa na OSHA kwa Maafisa ya Wizara, Mashirika ya Umma, Idara na Taasisi za serikali, Leo tarehe 25 Oktoba, 2022 Jijini Dodoma.

Mhe. Prof. Ndalichako, ameipongeza OSHA kwa kutekeleza maagizo ya Ofisi yake ambapo awali iliwaagiza kufanya ukaguzi katika ofisi zote za serikali na kisha kutoa mafunzo na ushauri wa kitaalam juu ya uboreshaji wa mazingira ya kazi katika ofisi hizo pamoja na miradi ya ujenzi inayoendelea.

“Ni matarajio yangu kwamba baada ya mafunzo haya mtapata uelewa wa kutosha kuhusu Sheria ya Afya na Usalama Mahali pa Kazi na mtaweza kwenda kuisimamia vizuri."

Amewataka wakawe mabalozi wa OSHA na wawasaidie kuwaelekeza wafanyakazi wachukue tahadhari kwani wanaweza kuwapa vifaa vinavyotakiwa lakini wakavitumia tofauti na maelekezo ya kitaalam.

"Niwapongeze OSHA kwa kutekeleza maagizo niliyowapatia mwezi Aprili lakini ningependa kuona mnawafikia wadau wengi zaidi na hata baadae mnaweza kupanga kuwakutanisha Makatibu Wakuu kwa ajili ya kuwapa elimu hii ili kurahisisha utekelezaji wa masuala haya"

Akizungumza wakati wa ufunguzi huo wa mafunzo, Mtendaji Mkuu wa OSHA, Khadija Mwenda amesema mafunzo hayo ni sehemu ya mrejesho wa kampeni ya ukaguzi na uchunguzi wa afya za wafanyakazi uliyoendeshwa na Taasisi yake mwezi Aprili mwaka huu na kubaini changamoto za usalama na afya ikiwemo uelewa mdogo miongoni mwa wadau.

Aidha, Mwenda ameeleza kuwa kupitia mafunzo hayo kutakuwa na uelewa wa pamoja miongoni mwa watendaji wa serikali na hivyo kuwezesha utoaji wa huduma kwa wananchi katika ofisi za umma pamoja miradi ya serikali kufanyika kwa kuzingatia kanuni za usalama na afya.