Tanzania emblem
The United Republic of Tanzania

Prime Minister's Office

Labour, Youth, Employment and Persons with Disability

News

Kamati ya Bunge Yaipongeza Ofisi ya Waziri Mkuu kwa Kutekeleza Maagizo


KAMATI ya Kudumu ya Bunge ya Katiba na Sheria, imepongeza Ofisi ya Waziri Mkuu, Kazi, Vijana, Ajira na Wenye Ulemavu kwa kutekeleza maagizo ya kamati hiyo huku ikishauri masuala mbalimbali ikiwamo kuwezesha nguvu kazi kupata ujuzi ili kuondokana na tatizo la ajira.

Pongezi hizo za kamati zimetolewa leo Januari 18, 2023 kwenye kikao cha kupokea na kujadili taarifa ya Ofisi hiyo kuhusu utekelezaji wa maazimio ya Bunge yaliyotokana na taarifa ya mwaka ya shughuli za kamati hiyo kwa kipindi cha Januari, 2021 hadi Februari, 2022 na utekelezaji wa bajeti ya Ofisi hiyo kwa Kipindi cha nusu Mwaka (Julai hadi Desemba, 2022).

Akizungumza kwenye kikao hicho, Makamu Mwenyekiti wa kamati hiyo, Mhe.Najma Murtaza Giga, amesema Ofisi hiyo imekuwa ikichukua ushauri wa kamati na kuufanyia kazi ipasavyo.

Naye, Mjumbe wa kamati hiyo ambaye ni Mbunge wa Mlalo, Mhe. Rashid Shangazi, amesema pamoja na jitihada zinazofanywa na Ofisi hiyo katika kuwezesha nguvu kazi kupata ujuzi ni vyema kuangalia zaidi fursa za ajira za ujuzi mbalimbali zilizopo nje ya nchi ili kutatua changamoto ya ajira nchini.

Kadhalika, Mjumbe wa kamati hiyo ambaye pia ni Mbunge wa Viti maalum, Mhe. Zainab Katimba, amepongeza wizara hiyo kwa kuimarisha mafunzo kwa vitendo kwa vijana na kushauri kuendelea kupanua wigo zaidi.

Awali, akiwasilisha taarifa za ofisi hiyo, Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu, Kazi, Vijana, Ajira na Wenye Ulemavu, Mhe. Prof. Joyce Ndalichako, amesema Ofisi imetekeleza maazimio ya kamati ikiwamo kuimarisha mfumo wa uratibu ajira za watanzania nje ya nchi ikiwa ni pamoja na kuanza kutumia mfumo wa kielektroniki katika michakato ya kuwaunganisha watanzania na fursa hizo.

“Agizo jingine lilikuwa ni vijana wenye Ulemavu wajumuishwe kwenye programu ya kukuza ujuzi pamoja na kwenye mkakati wa ajira katika miradi mbalimbali nchini, suala hili limetekelezwa na tumezindua muongozo wa utekelezaji, ujumuishwaji na uimarishaji wa huduma kwa Watu wenye Ulemavu wa mwaka 2022,” amesema

Waziri Ndalichako ameiahidi kamati hiyo kuwa Ofisi yake itaendelea kufanyia kazi mapendekezo yaliyotolewa kwa ubunifu.

Akijibu hoja mbalimbali za wajumbe wa kamati hiyo, Katibu Mkuu wa Ofisi hiyo, Mhe. Prof. Jamal Katundu, amesema asilimia 50 ya vijana wa mafunzo tarajali wanaopelekwa kwenye sekta binafsi wamekuwa wakipata ajira kabla ya kumaliza muda wa mafunzo hayo.

“Ofisi ya Waziri Mkuu tuna utaratibu mzuri wa kuwasaidia vijana ambao hawana uzoefu wanapata uzoefu kupitia programu ya kukuza ujuzi,” amesema

Aidha, amesema Ofisi imejipanga kuhakikisha mapitio ya sera ya vijana yanakamilika ndani ya mwaka huu wa fedha.

Kuhusu ulipaji wa mafao kwa wastaafu, Katibu Mkuu huyo amesema kuna maboresho makubwa yamefanyika na sasa wastaafu wanalipwa mafao yao ndani ya siku 60.

Pamoja na mambo mengine, Wajumbe wa kamati hiyo wamewapongeza Watendaji na Wakurugenzi wa taasisi zilizo chini ya Ofisi hiyo ambazo ni Wakala wa Usalama na Afya Mahala pa Kazi (OSHA), Mfuko wa Taifa wa Hifadhi ya Jamii (NSSF), Mfuko wa hifadhi ya jamii kwa Watumishi wa Umma (PSSSF), Mfuko wa Fidia kwa Wafanyakazi (WCF) na Tume ya Usuluhishi na Maamuzi (CMA) kwa kuendelea kufanya kazi kwa ufanisi na kuzingatia maoni ya kamati.