Tanzania emblem
The United Republic of Tanzania

Prime Minister's Office

Labour, Youth, Employment and Persons with Disability

News

Serikali imeanza kufanyia kazi maboresho ya Mishahara Vyuo Vikuu - Mhe. Katambi


SERIKALI imeanza kufanyia kazi suala la maboresho ya mishahara kwenye vyuo vikuu kupitia Ofisi ya Waziri Mkuu na Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia.

Naibu Waziri, Ofisi ya Waziri Mkuu, Kazi, Vijana, Ajira na Wenye Ulemavu, Mhe. Patrobas Katambi, ameyasema hayo leo bungeni alipokuwa akijibu maswali ya nyongeza Mbunge wa Viti maalum, Mhe. Dkt.Thea Ntara ambaye ameuliza mchakato wa mkataba namba 189 umefikia wapi ili kuboresha mishahara ya wafanyakazi wa majumbani na pia amehoji kuboresha mishahara kwa wakuu wa vyuo vikuu.

Akijibu maswali hayo, Mhe.Katambi amesema suala hilo la maboresho la mishahara linaangalia viwango kulingana na hali ya kiuchumi na uhalisia wa kidunia wa sasa.
Aidha, amesema Serikali ilishaanza kuufanyia kazi mkataba wa kimataifa namba 189 ikiwa ni maelekezo ya Mhe.Rais Dkt.Samia Suluhu Hassan.

Amesema mkataba huo kuna vipengele bado vinaendelea kufanyiwa kazi ambavyo vipo vinavyoendana na hali ya uchumi na uhalisia wa kimazingira na kitamaduni.

“Serikali inaendelea kuzichukua hizo hatua zote kwa haraka na naimani katika kipindi cha mwaka huu wa fedha hayo yote tutakuwa tumeweza kuyaangalia hasa kuhusu haki na stahiki za mikataba ya wafanyakazi wa ndani,”amesema.

Mhe.Katambi amesema serikali kupitia Kamishna wa Kazi inaangalia ili kuona namna ya kutengeneza viwango vinavyoendana na nchi za kuangalia maslahi kwenye kundi hilo.
Awali, katika swali la msingi, Mbunge huyo amehoji lini Serikali itatangaza kima cha chini cha mshahara kwa Wafanyakazi wa serikali na mashirika binafsi.

Mhe.Katambi akijibu swali hilo, amesema kima cha chini cha mshahara kwa sekta ya umma kilitangazwa Mei 13, 2022 na utekelezaji wake umeanza Julai mosi mwaka 2022 na kwa sekta binafsi kima hicho kilitangazwa Novemba 25, 2022 baada ya Bodi ya Kima cha Chini cha Mishahara kukamilisha utafiti na kutoa mapendekezo ya viwango kwa sekta hiyo ambayo yaliridhiwa na Baraza la Ushauri kuhusu Kazi, Uchumi na Jamii (LESCO) na utekelezaji wake ulianza rasmi Januari mosi, 2023.