Tanzania emblem
The United Republic of Tanzania

Prime Minister's Office

Labour, Youth, Employment and Persons with Disability

News

SERIKALI YA AWAMU YA SITA IMEFANYA MAGEUZI MAKUBWA KATIKA SEKTA YA KAZI NA AJIRA – WAZIRI MHAGAMA


Serikali ya Awamu ya Sita inayoongozwa na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Samia Suluhu Hassan imefanya mageuzi makubwa katika sekta ya Kazi na Ajira kwa kujenga mazingira ya kuvutia wawekezaji nchini ambayo yamekuwa ni chachu ya kukuza pato la taifa sambamba na kuongeza fursa za ajira.

Hayo yameelezwa na Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu anayeshughulikia masuala ya Sera, Uratibu, Bunge, Kazi, Vijana, Ajira na Wenye Ulemavu Mhe. Jenista Mhagama alipotembelea Banda la Ofisi yake pamoja na Mabanda ya Taasisi zilizopo chini ya Ofisi hiyo katika Maonesho ya 45 ya Biashara ya Kimataifa ya Dar es Salaam Julai 5, 2021, Jijini Dar Es Salaam.

Waziri Mhagama alieleza kuwa Serikali anayoiongoza Mhe. Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania imedhamiria kufanya mageuzi makubwa katika sekta ya kazi na ajira ambapo Ofisi ya Waziri Mkuu imeendelea kuunga mkono juhudi za serikali ya Awamu ya Sita kwa kujenga mazigira wezeshi ambayo yamekuwa yakivutia zaidi wawekezaji kuja kuwekeza nchini.

“Ndani ya siku mia moja za utawala wake Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Samia Suluhu Hassan Ofisi ya Waziri Mkuu imefanikiwa kutekeleza maagizo ya Mhe. Rais kwa kuweka mifumo mizuri inayohamasisha zaidi uwekezaji nchini pamoja na kulinda ajira za wazawa (Watanzania),” alieleza Waziri Mhagama

Aliongeza kuwa Ofisi hiyo imebadili muundo wa kiutendaji wa utoaji wa vibali vya Ajira na Ukaazi kwa wageni ambao hivi sasa mfumo unaotumika ni wa kidigitali ambayo ni njia bora ya kupunguza urasimu na kuhakikisha kunakuwa na uwekezaji wenye tija.

“Mfumo huu mpya wa kielektroniki wa vibali vya kazi na ukaazi kwa wageni umesaidia kupuguza hatua kutoka 33 hadi hatua saba (7) ambazo zilikuwepo hapo awali, hivyo Serikali imefanya utoaji wa vibali kwa wageni kuwa rahisi” alisema Mhagama

“Mfumo wa maombi ya vibali kwa njia ya kidigitali umepunguza gharama na mfumo huo umekuwa ni sehemu ya kupunguza na kuondosha vikwazo vya uwekezaji ili kuvutia wawekezaji wengi zaidi hapa nchini, leo hii siku za kutoa kibali hicho zimepungua kutoka 14 hadi siku tatu (3),” Alieleza

Alifafanua kuwa katika kuweka mazingira mazuri ya uwekezaji nchini Serikali imeendelea kufanya mageuzi makubwa ya Kisheria ambazo zitawalinda watanzania kupitia uwekezaji wa aina mbalimbali sambamba na kuwarithisha watanzania ujuzi wa wageni wanaoomba vibali.

Sambamba na hayo Waziri Mhagama alisema kuwa Serikali imeshakamilisha utafiti wa hali ya nguvu kazi nchini kwa lengo la kutambua nguvu kazi ya aina gani inayoitajika nchini, ujuzi upi unatakiwa kutolewa ili kuleta mageuzi makubwa ya kiuchumi katika Taifa.

Katika Ziara hiyo Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu anayeshughulikia masuala ya Sera, Uratibu, Bunge, Kazi, Vijana, Ajira na Wenye Ulemavu Mhe. Jenista Mhagama alitembelea Banda la Ofisi yake pamoja na Mabanda ya Taasisi zilizopo chini ya Ofisi hiyo ikiwemo Mfuko wa Hifadhi ya Jamii kwa Watumishi wa Umma (PSSSF), Shirika la Taifa la Hifadhi ya Jamii (NSSF), Mfuko wa Fidia kwa Wafanyakazi (WCF) na Wakala wa Usalama na Afya Mahala Pa Kazi (OSHA). Pia Waziri Mhagama alitembelea Banda la Ofisi ya Bunge.

Mara baada ya kutembelea mabanda hayo Waziri Mhagama amepongeza Ofisi yake na Taasisi zilizopo chini ya Ofisi hyo kwa maandalizi mazuri na pia amewahimiza watoe huduma bora na elimu ya kutosha kwa wananchi.

Kauli Mbiu ya Maonesho hayo ya 45 ya Biashara ya Kimataifa ya Dar es salaam isemayo “Uchumi wa Viwanda kwa Ajira na Biashara Endelevu”.