Tanzania emblem
The United Republic of Tanzania

Prime Minister's Office

Labour, Youth, Employment and Persons with Disability

News

Serikali Yaahidi Kuendelea Kulinda na Kusimamia Haki za Watu wenye Ulemavu


Serikali imeahidi kuendelea kusimamia na kulinda haki za Watu wenye Ulemavu nchini ili kuwezesha kundi hilo kuwa na ustawi mzuri katika nyanja mbalimbali.

Kauli hiyo imetolewa Februari 25, 2022 na Naibu Waziri Ofisi ya Waziri Mkuu anayeshughulikia Kazi, Vijana, Ajira na Wenye Ulemavu Mhe. Patrobas Katambi wakati akifunga Kikao cha Kurekebisha Mpango Kazi wa Taifa kwa Watu Wenye Ualbino 2022/2023 - 2026/2027 (National Action Plan for Persons with Albinisms - NAP) kilichofanyika Dodoma Hotel, Jijini Dodoma.

Naibu Waziri Katambi alieleza kwamba Ofisi ya Waziri Mkuu itaendelea kushirikiana na wadau wanaotoa huduma kwa Watu wenye Ulemavu ili kuhakikisha utekelezaji wa Sera, Sheria, Miongozo na Mikataba ya Kimataifa ambapo utekelezaji wake utasaidia jamii kutambua haki na wajibu wa Watu wenye Ulemavu.

“Kwa muda mrefu kundi la Watu wenye Ualbino limekuwa katika wakati mgumu wa kufanyiwa vitendo vya kikatili ambavyo vilichangia kuzorota kwa maendeleo yao ya kijamii na kiuchumi, hivyo kuandaliwa kwa mpango huu utasaidia kuweka mikakati endelevu ya utekelezaji wa changamoto zote ambazo wamekuwa wakikabliana nazo,”

“Mpango Kazi huu wa Taifa kwa Watu wenye Ualbino ni faraja kubwa sana kwetu sisi kama Serikali pamoja na wadau kwa sababu mpango huu umeweka bayana maeneo makuu manne ambayo ni ulinzi, uzuaiji, usawa, ubaguzi na uwajibikaji,” alisema Mhe. Katambi.

Aliongeza kuwa, Serikali inaendelea kutoa kipaumbele katika huduma za afya kwa Watu wenye Ulemavu, kuboresha miundombinu ili kujenga mazingira fikivu yatakayo wawezesha Watu wenye Ulemavu kufanya shughuli zao katika mazingira rafiki kama watu wengine.

“Serikali inatekeleza miradi mbalimbali na katika ujenzi wa miradi hiyo inazingatia miundo mbinu rafiki kwa Watu wenye Ulemavu ili wawezesha kupata huduma kama watu wengine na wamekuwa wakipewa kipaumbele wanapoenda kupata matibabu au huduma nyingine za kijamii mahali popote,” alieleza

Vilevile alibainisha kwamba Watu wenye Ulemavu wana haki ya kushiriki katika shughuli mbalimbali za kiuchumi ikiwemo fursa za ajira au fursa mbalimbali zinazojitokeza ili wajikwamue kiuchumi badala ya kuendelea kuwa tegemezi, hivyo alihasa jamii kutambua mchango wa Watu wenye Ulemavu kuanzia ngazi ya familia hadi Taifa kwa ujumla.

Kwa upande wake Katibu Mkuu wa Chama cha Watu wenye Ualbino Tanzania (TAS) Bw. Mussa Kabimba alitumia fursa hiyo kuishukuru Serikali kwa kushirikiana na chama hicho cha TAS pamoja na wadau katika uaandaji wa mchakato huo hadi kufikia hatua ya kukamilika kwake.

“Tunashukru watalamu wote kutoka Ofisi ya Waziri Mkuu kupitia kitengo cha huduma kwa Watu Wenye Ulemavu na Idara ya Sera na Mipango kwa namna walivyojitoa kushirikiana pamoja na Chama cha Watu wenye Ualbino Tanzania (TAS) katika kurekebisha Mpango kazi huu wa Taifa kwa Watu wenye Ualbino,” alisema

Pamoja na hayo, alitumia fursa hiyo kupongeza mchakato wa Serikali wa ujenzi wa Vyuo vipya vya Ufundi Stadi kwa Watu wenye ulemavu katika mkoa wa Kigoma na Songwe sambamba na maboresha ya vyuo sita vya Ufundi Stadi kwa watu wenye ulemavu ambavyo ni Yombo - Dar es salaam, Mtapika - Mtwara, Sabasaba - Singida, Luanzari - Tabora, Masiwani – Tanga na Milongo kilichopo Jijini Mwanza.

Naye Makamu Mwenyekiti wa Shirikisho la Vyama vya Watu wenye Ulemavu (SHIVYAWATA) Bi. Tungi Mwanjara alihimiza Serikali kushirikiana na wadau wa maendeleo kutoa elimu kuhusu haki za Watu wenye Ulemavu ili kuhakikisha usalama wa kundi hilo.