Tanzania emblem
The United Republic of Tanzania

Prime Minister's Office

Labour, Youth, Employment and Persons with Disability

News

VIJANA WATAKIWA KUTUMIA MAFUNZO YA UFUNDI STADI KUAJIRIKA KUJIAJIRI NA KUAJIRI WENZAO


Vijana wameaswa kuthamini na kutumia ipasavyo fursa ya mafunzo ya ufundi stadi yanayoratibiwa na Ofisi ya Waziri Mkuu kwa kuwa ni nyenzo muhimu ya kuwawezesha kuajirika, kujiajiri na kuajiri wenzao.

Hayo ameelezwa Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu anayeshughulikia masuala ya Sera, Bunge, Kazi, Vijana, Ajira na Wenye Ulemavu Mhe. Jenista Mhagama wakati wa ziara yake ya kikazi alipokuwa akikagua maendeleo ya mafunzo ya Uanagenzi yanayoratibiwa na Ofisi yake katika Mamlaka ya Elimu na Mafunzo ya Ufundi Stadi (VETA), Mkoani Lindi.

Waziri Mhagama alieleza kuwa, Serikali kupitia Ofisi ya Waziri Mkuu – Sera, Uratibu, Bunge, Kazi, Vijana, Ajira na Wenye Ulemavu kwa kushirikiana na wadau mbalimbali inatekeleza Programu ya Taifa ya Kukuza Ujuzi nchini ambayo inalenga kuimarisha nguvukazi iliyo katika soko la ajira kwa kuipatia ujuzi na stadi za kazi.

“Serikali ya Awamu ya Sita inayoongozwa na Mhe. Samia Suluhu Hassan Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania imeendelea kuwatengenezea vijana mfumo maalumu wa kupata ujuzi ili waweze kuondokana na changamoto ya ajira kwa kuwapatia mafunzo yenye ujuzi staki unaohitajika katika soko la ajira,” alisema Mheshimiwa Mhagama

Alifafanua kuwa chimbuko la Programu hiyo ya Kukuza Ujuzi ilitokana na changamoto iliyoibuliwa na waajiri kwamba mara nyingi wameshindwa kuwaajiri wahitimu wa ngazi mbalimbali kwa sababu ya kukosa ujuzi wa kutekeleza kazi za fani walizosomea, hivyo serikali kwa kushirikiana na sekta binafsi iliandaa programu hiyo kwa lengo la kukuza ujuzi kwa nguvukazi nchini katika fani mbalimbali.

“Utafiti wa Nguvukazi wa mwaka 2014 ulibainisha kuwa takribani asilimia 3.6 ya nguvukazi ya Taifa ina kiwango cha juu cha Ujuzi, asilimia 16.6 ina kiwango cha kati cha ujuzi na asilimia 79,9 ya nguvu kazi ina kiwango cha chini cha ujuzi,” alifafanua

“Katika mpango wa miaka mitano (5) wa maendeleo serikali imejikita katika kuipatia nguvukazi ujuzi ili kuwa na kiwango cha ujuzi kinachokubalika kwa ujuzi wa kiwango cha chini kufikia asilimia 54, ujuzi wa kati asilimia 34 na ujuzi wa juu asilimia 12,” alieleza

Alieleza kuwa mafunzo hayo yamekuwa na mchango mkubwa kwa vijana hususan katika kuongezeka kwa fursa za ajira na uwezo wa kuajirika pamoja na baadhi yao wamepata ajira kwenye miradi ya kimkakati ya maendeleo inayotekelezwa na Serikali.

“Awamu ya kwanza tulitoa mafunzo kwa vijana ya fani mbalimbali, hii leo wapo vijana waliosomea fani ya ufundi magari wamefungua karakana yao katika Kijiji cha Nyengedi wanatengeneza magari na pikipiki ambazo hapo awali zilikuwa zikitengenezwa mjini. Vilevile vijana hao wameweza kutoa fursa ya ajira kwa vijana wenzao,” alisema Mhagama

“Kijana wengine alisomea fani ya upishi katika chuo cha VETA hapa lindi leo hii ni mpishi mkuwa katika hoteli maarufu ya hapa lindi inaitwa Sea View, hivyo programu hii imekuwa na manufaa makubwa kwa vijana nchini, niwasii vijana kuthamini fursa hiyo waliyopewa na serikali yao pamoja na kuzingatia mafunzo wanayopatiwa” alisema Mhagama

Aidha, Waziri Mhagama ametaka Ofisi yake kwa kushirikiana na vyuo vya Ufundi stadi nchini kuhakikisha kozi wanazotoa kwa vijana ziweze kurandana na aina ya uchumi uliopo katika maeneo yanayowazunguka kusudi vijana waweze kuajirika kwenye miradi inayoanzishwa katika maeneo yao.

Sambamba na hayo amezitaka Halmashauri zote nchini kuwa na kanzi data ya vijana wanaopatiwa mafunzo ya ufundi stadi katika meneo yao ili fursa zinapojitokeza waweze kutoa kwa vijana hao.

“Mheshimiwa Rais na Mama yetu Samia Suluhu Hassan amekuwa akitoa fedha kwa ajili ya miradi mingi ikiwemo Ujenzi wa Barabara, Shule na Vituo vya Afya. Kupitia fursa hizo ni bora mkatumia vijana hao katika miradi hiyo kwa kuwa wanauwezo na ujuzi tayari waliojengewa na serikali,” alieleza

Pia ameziagiza Halmashauri kutoa mikopo kwa wingi ya asilimia 4 kwa vijana inayotokana na mapato ya ndani ili vijana waweze kuanzisha miradi au shughuli mbalimbali za kiuchumi zitakazo wawezesha kujiajiri na kuajiri wenzao.

Naye Mnufaika wa Mafunzo hayo Ndg. Juma Mussa wameishukuru Serikali kwa kuendelea kuwajali na kutambua mchango wa vijana katika jamii kwa kuwapatia ujuzi ambao utakuwa na manufaa katika kuwawezesha kuondokana na changamoto ya ajira.

“Tunamshukuru Rais wetu Mhe. Samia Suluhu Hassan pamoja na wasaidizi wake kwa kutupatia fursa hii, sisi vijana tutasoma kozi zetu vizuri ili tutakapomaliza tulitumikie taifa letu,” alisema Mussa