Tanzania emblem
The United Republic of Tanzania

Prime Minister's Office

Labour, Employment and Relations

News

Waziri Sangu Ahimiza Nidhamu na Uwajibikaji kwa Wafanyakazi wa Kitanzania Nchini Qatar


Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu – Kazi, Ajira na Mahusiano, Mhe. Deus Sangu, amewahimiza Watanzania wanaofanya kazi nchini Qatar kuzingatia nidhamu, uwajibikaji na uadilifu wanapotekeleza majukumu yao ili kuendelea kujenga taswira nzuri ya Taifa la Tanzania na kufungua fursa zaidi za ajira na maendeleo kwa Watanzania wengine.

Mhe. Sangu ametoa wito huo tarehe 8 Julai 2026, jijini Doha, Qatar, alipokutana na kuzungumza na Wafanyakazi Madereva wa Kitanzania wanaofanya kazi katika kampuni ya MOWASALAT iliyopo nchini humo, ambapo alisisitiza umuhimu wa kufuata sheria, kuheshimu mikataba ya ajira na kutekeleza majukumu kwa weledi.

Amesema kuwa mafanikio yanayoendelea kupatikana kwa Watanzania katika nchi mbalimbali yanatokana na juhudi, kujituma na kuonesha uwezo katika maeneo yao ya kazi.

“Uwepo wa Watanzania wanaofanya kazi katika mataifa ya nje kwa bidii ni sifa kubwa kwa taifa, kwani inasaidia kujenga imani na mahusiano mazuri kati ya Tanzania na mataifa mengine, hivyo kutoa fursa zaidi kwa vijana wengine kupata nafasi za ajira na kujifunza,” amesema Waziri Sangu

Ameongeza kuwa Serikali ya Awamu ya Sita inayoongozwa na Mhe. Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan itaendelea kuweka mazingira wezeshi ya kuongeza fursa za ajira na kuimarisha ushirikiano wa kimataifa katika masuala ya ajira na kukuza maendeleo ya rasilimali watu.

Vile vile, Waziri Sangu amewataka Watanzania hao kuendelea kushirikiana na viongozi wa Serikali hususan Ofisi za Ubalozi, ili kupata mwongozo na msaada pale inapohitajika kuhusiana na masuala ya kisheria, kanuni na taratibu za nchi wanayoishi.

Kadhalika, Mhe. Sangu amewahamasisha madereva hao kuendelea kuwa mabalozi wazuri wa kulitangaza taifa la Tanzania kupitia juhudu zao katika kazi. Pia, amewahamasisha kujiunga katika Mfuko wa Taifa wa Hifadhi Jamii (NSSF) kupitia Hifadhi Scheme ili kujijengea usalama wa kipato na ustawi wa maisha yao baada ya kustaafu au wanapokumbwa na changamoto mbalimbali za maisha, kwa kuwa hatua hiyo ni uwekezaji muhimu kwa manufaa yao binafsi na familia zao.

Nye, Balozi wa Tanzania nchini Qatar, Mhe. Habibu Awesi Mohamed amewahakikishia wafanyakazi hao kupatiwa ushirikiano wakati wowote watakapokuwa wanahitaji kupata huduma, ushauri na msaada mbalimbali wanapokuwa katika nchi hiyo.

Kwa upande wa Madereva hao wakizungumza kwa nyakati tofauti, wameshukuru Serikali kwa kuwaunganisha na fursa za ajira nje ya nchi. “Tunaishukuru sana Serikali kwa kutufungulia milango ya ajira nje ya nchi. Tunaomba juhudi hizi ziendelezwe ili vijana wengi zaidi waliopo Tanzania wapate fursa kama tulizopata sisi kwa kuwa zitaboresha maisha yao pamoja na kuwawezesha kuchangia maendeleo ya Taifa,” amesema Zulekifli Ali Massawe